Sababu saba (7) zinazofanya wasomaji wanunue au wasinunue vitabu.
Kila mwandishi wa vitabu hutaka sana kuona kitabu chake kinanunulika na kufikia wasomaji wengi wa vitabu. Kitabu kununulika au kutonunulika imekuwa ni kama kipimo cha mafanikio kwa mwandishi kujua kazi yake imepokelewaje na wasomaji. Lakini yako mambo mengi yanayochangia wasomaji kununua kitabu cha mwandishi fulani na si mwandishi fulani.
Buinda Mjungu ni msomaji nguli wa vitabu na kwa sababu ya usomaji wake amebatizwa jina la malkia wa vitabu na waandishi wa vitabu. Katika ukurasa wake wa Facebook aliandika uzoefu wake kuelezea sababu zinazofanya wasomaji wanunue kitabu hiki na sio kile. Buinda anataja sababu saba zifuatazo;
1. Nilisema kuwa watu huwa wanavutika kununua kitabu kutokana na jina lake tu kumvutia au kumjengea udadisi hivyo kujua ndani kuna nini.
2. Kuna wengine wanavutiwa na jalada la kitabu, hicho tu kinamhamasisha kununua. Kuna kitabu fulani niliwahi kukinunua kina riwaya nzuri ila picha ya jalada lake linaogopesha hasa ukistuka usiku na kulitazama. Kilinipa shida sana kukisoma hadi ikabidi nifunike jalada ndipo nikisome na hata binti yangu kilikuwa kinamtisha hadi akaniambia nikifiche.
Bahati nzuri niliongea na mwandishi na nikamuelezea hiyo picha ya jalada itakavyoathiri biashara yake hasa pia baada ya kupokea malalamiko mengi ya watu, yaani hata kukitangaza nilishindwa. Ila mwandishi alinielewa na kubadilisha picha ya jalada na sasa watu hawaogopi kukinunua nami namsubiri anibadilishie kitabu kingine.
3. Kuna watu wengine wananunua kitabu kutokana na jina la mwandishi. Mwingine kwa kuwa anafahamika sana au ni rafiki yao basi na kitabu chake kinakuwa kinauzika lakini sio kwamba kinasomwa sana. Kuna baadhi ya watu waliwahi kununua kitabu fulani na wakawa wanakisifia, nikawafuata kuwaambia wanisimulie kitabu kikoje ili nihamasike kununua (sio kwamba sikuwa nacho), wakaniambia "Kwani tumekisoma basi, huwa hatusomi vitabu vya aina hiyo ila tumenunua kumtia moyo tu"
4. Wengine wananunua kitabu kutokana na aina ya matangazo
- Kwamba kitabu kinatangazwa vipi
- Nani wanakitangaza
- Hamasa ya jamii ikoje
- Waliokinunua/kukisoma wanakizungumziaje
5. Wengine wanunua kitabu kutokana na aina ya kitabu, kwamba kinazungumzia nini, hicho kilichoandikwa kinatia hamasa, kuburudisha, kufundisha, kuburudisha, kufikirisha au kuna nini ndani
6. Wengine wanunua kitabu kutokana na kufuata mkumbo. Hawa sio wapenzi wa vitabu ila wanaangalia upepo unavyoenda. Wanaweza kununua kitabu cha mwandishi fulani ili tu mbeleni afanikishe mambo yake kupitia mwandishi huyo. Hawa hawawezi kununua kitabu kama hawafahamiani na mwandishi hata kama kitabu ni kizuri. Wanaweza kukuomba uwanunulie kitabu ukidhani wanapata hamasa ya kusoma kumbe wala, wao wana malengo yao na sio usomaji. Mara nyingi matarajio yao yasipofikiwa na zoezi la kuwa na vitabu linafikia tamati.
7. Wengine wanunua kitabu kwa sababu ni wasomaji/wapenzi wa vitabu. Amjue au asimjue Mwandishi atanunua ilimradi asake maarifa. Akikuta kitabu kwa wakala hata kama hakijatangazwa atanunua. Huyu hata akikuta kitabu hakina jalada wala jina la mwandishi atakisoma maana damuni mwake upo USOMAJI. Anaweza kuwa na chaguo maalum la vitabu au akanunua vya kila aina ila akajua kujidhibiti katika maarifa apatayo maana sio kila kitabu ni kizuri kwa afya ya akili, ukuaji kiroho, maadili, nk.
Imeandikwa na Malkia wa Vitabu, 09.08.2022 na kupitiwa na DL Bookstore.
Karibu kwa maoni yako hapa chini.