Vichaka
Mungu alipomuumba mwanadamu, kuna mahala ama majukumu alitegemea yafanyike kupitia yeye kama kuwakilishi wake rasmi kabisa hapa duniani. Ili jukumu hilo liweze kufanyika kwa ufanisi na kuleta matokeo tarajiwa, mwanadamu anapaswa kukaa katika nafasi hiyo wakati wote wa maisha yake.
Biblia katika kile kitabu cha Mwanzo 2:15 inasema, “Basi, Mwenyezi-Mungu akamtwaa huyo mwanamume, akamweka katika bustani ya Edeni, ailime na kuitunza.” hii inamaanisha kwamba, Mungu anampatia bustani iliyo kamili kama ambavyo mimi na wewe tumepewa maisha yaliyo kamili, yasiyo na mapungufu ya kimfumo.
Ni jukumu letu sasa kama lilivyokuwa kwa Adamu, kutunza na kulinda kile tulichopewa ama kukabidhiwa tena kwa kupewa na muongozo. Popote pale ambapo umakini wetu unapungua basi zoezi la kutunza huzorota na kutengeneza kitu kiitwacho kichaka jambo ambalo hubadili taswira ya kile tulichopewa, kuathiri utendaji, kualika uadui na vita, kupoteza muelekeo na kuzalisha majuto, aibu, fedheha na kilio.