Heshima kwa Wazee kichocheo cha mafanikio
Mafanikio; umekuwa msamiati pendwa kwa kila mmoja kutamani kufanikiwa na wengine wakienda mbali zaidi kwa kutamani mafanikio ya haraka kitu ambacho kimegharimu utu na maisha ya wengi, kwa upande mwingine mafanikio ni kitu kizuri cha kujivunia ikiwa kitatokea kwa kufuata utaratibu wa mafanikio.
Nduguyangu ni vyema ukatambua kuwa mafanikio hayatokei tu, mafanikio ni matokeo ya juhudi za kimakusudi za kufuata kanuni na taratibu za kufanikiwa, naweza kusema mafanikio ni mazao ya kufuata kanuni na taratibu za mafanikio. Kuna kanuni nyingi ambazo zinaweza kumsaidia mtu kufanikiwa katika chochote anachokusudia kufanikiwa mfano kitaaluma, kikazi, kibiashara, kifamilia n.k. Mojawapo ya kanuni hizo ni pamoja na kuwa na maono, kuweka malengo, nidhamu binafsi, kuwa na watu sahihi kwenye maisha, kuwa na heshima na mtazamo chanya n.k
Kwa mlengo wa kitabu hiki tunajikita katika kutambua siri moja ya mafanikio ambayo ni heshima na zaidi tutaangalia heshima kwa wazee wetu na namna ambavyo inaweza kimaalumu kabisa kumsaidia mtu kufanikiwa katika mambo mbalimbali ikiwepo kitaaluma, kiuchumi, kifamilia na kimaisha kwa ujumla
Ili kuzuia madhara ya kuwa na jamii isiyothamini wazee wala kuwaheshimu ambayo ni nidhamu na maadili kuzidi kuporomoka na mafanikio kubaki kuwa ndoto isiyotimia kwa wengi ni vizuri tukajifunza zaidi jambo hili.
Ukizingatia kuwa mafanikio ni ndoto ya kila mtu lakini ili ndoto hii iweze kutimia kuna namna ya mtu anatakiwa kuwa ili kuchochea mafanikio yake na mojawapo ya kichocheo hicho ni kutambua nafasi ya wazee na kuwapa heshima wanayostaili.
Kitabu hiki kimelenga kupanua uelewa wa mtu binafsi na jamii kuhusu heshima kwa wazee kwa kutambua ikiwa wazee wetu watapata heshima wanayostahili itakuwa vyepesi sana kuheshimu wakuu wetu wa kazi, wafanyakazi wenzetu, familia na hivyo kuwa katika nafasi nzuri ya kufanikiwa.
Recommended for you


